- Home
- About Us
- Organization Structure
- Board of Trustees
- Rector
- Gallery
- Publications
- Students Welfare
- Campuses
Timu ya mpira wa pete (Netball) ya Chuo cha Serikali za Mitaa leo imechukua ubingwa wa Mashindano ya Shirikisho la Michezo la Vya Elimu ya Juu Tanzania (SHIMIVUTA) 2022 kwa kuwafunga Chuo Cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) kwa magoli 41 – 33 katika fainali iliyofanyika viwanja vya Chuo cha Ualimu Butimba jijini Mwanza.
Huku wakionesha kutoa upinzani Chuo cha Mipango lakini mambo yalikuwa magumu kwao kuwakabili Chuo cha Serikali za Mitaa wakiongozwa na Nahodha wao Glory kwani katika robo zote nne walizocheza LGTI waliongoza robo tatu na Mipango wakiongoza kwenye robo ya mwisho tu. Katika robo ya kwanza LGTI 10 Mipango 6, robo ya pili LGTI 10 Mipango 8, robo ya tatu LGTI 15 Mipango 8 na robo ya nne LGTI 6 Mipango 11.
Akizungumza baada ya Mchezo huo wa fainali Nahodha Msaidizi wa LGTI Suzana Ndondi alisema kuwa kwa mwaka huu timu zimejiandaa kuliko miaka ya nyuma lakini wao walikuwa wamejiandaa vizuri Zaidi ndo maana wakachua ubingwa.
“Kwa kweli mwaka huu ulikuwa tofauti na miaka ya nyuma, mwaka huu timu zimefanya maandalizi sana kwani hata hawa Mipango tuliocheza nao leo tofauti na wale tuliocheza nao fainali mwaka jana kule Iringa kwani mwaka jana tuliwafunga 60 – 20 lakini mwaka huu wameonesha kubadilika sana” Alisema Suzana.
Kwa upande wao wachezaji wengi wa Mipango wamekubaliana na matokeo hayo kwa kueleza kuwa wenzao wamewazidi uzoefu na kusema kuwa watajipanga kwa mashindano ya mwakani.
Hii ni mara ya tatu mfululizo kwa Chuo cha Serikali za Mitaa kuchukua Ubingwa wa SHIMIVUTA kwani walichukua 2020,2021 na sasa wamechukua tena 2022.
Wakati huo huo Timu ya mpira wa miguu ya Chuo cha Serikali za Mitaa nayo imeshika nafasi ya pili katika mashindano hayo mara baada ya kupoteza mchezo wake wa fainali kwa magoli 2 – 1 dhidi ya Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) katika mchezo uliochezwa katika uwanja wa Nyamagana jijini Mwanza.
Kwa kupoteza mchezo huo LGTI imeshika nafasi ya pili tofauti na mwaka jana ambapo alishika nafasi ya nne.
Akizungumzia matokeo hayo Kocha Mkuu wa timu ya Chuo cha Serikali za Mitaa Ashrafu Athumani alisema timu yake imejitahidi sana kwa kushika nafasi ya pili kwani tangu ianze kushiriki mashindano hayo haijawahi kucheza fainali na kuahidi Kwenda kuiandaa vizuri timu kwa ajili ya mashindano yam waka 2023.
“Nawapongeza wachezaji wangu kwa kuonesha kiwango kikubwa sana tangu mwanzo wa mashindano haya hadi leo tumefika fainali, kikubwa tumejifunza namna ya kucheza fainali na kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu mwakani tunaweza kuwa vizuri Zaidi japokuwa tunajua na wenzetu watajinga” Alisema Kocha Ashrafu.
Vilevile katika mashindano hayo wachezaji mbalimbali wa LGTI walijinyakulia medali mbalimbali za riadha kwa meta 100,400, 3000, 5000 na mbio za vijiti.
Mara baada mashindano hayo kufungwa rasmi Kaimu Naibu Mkuu wa Chuo Cha Serikali za Mitaa Daktari Lazaro Kisumbe na Rais wa Serikali ya Wanafunzi (LOGISO) Bwana Samalu Girehe waliandaa tafrija ya chakula cha jioni na kuwapongeza wanamichezo wote waliokuja jijini Mwanza kushiriki michezo hiyo.
“Kwanza kabisa niwapongeze wote kwa kushiriki na kumaliza michezo salama na pia niwapongeze kwa kushinda nafasi mbalimbali katika mashindano, kwa kufanya hivi mmekitangaza sana Chuo chetu kuwa zaidi ya kutoa elimu lakini pia chou kinashiriki katika michezo mbalimbali na kina hadi wachezaji wa timu ya Taifa” Alisema Dkt.Kisumbe.
“Nimeongea na Mkuu wa Chuo Dkt. Mashala kuhusu ushindi huu na amewaahidi kuangalia namna ya kuwafanyia sherehe ya kuwapongeza kwa hiki mlichokifanya mara mtakaporudi Chuoni hasa baada ya sikukuu za mwisho wa mwaka kupita” Aliongeza Dkt. Kisumbe.
Mashindano hayo hufanyika kila mwaka na kwa mwaka huu yameshirikisha vyuo 20 vikiwemo Chuo Cha Serikali za Mitaa (LGTI) , Chuo Kikuu cha Dar es salam (UDSM), Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (SUA), Chuo cha Maendeleo ya Mipango Vijijini (IRDP), Chuo Cha Usimamizi wa Fedha (IFM), Chuo cha Diplomasia (CFR), Chuo Cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Chuo cha Usafirishaji (NIT) ,Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA), Chuo cha Uhasibu Tanzania (TIA), Chuo cha Ufundi Arusha (ATC),Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Chuo Cha Ustawi wa Jamii Kijitonyama (ISW), Chuo cha Maendeleo ya Jamii Tengeru (TICD), Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima Tanzania (IAE) , Taasisi ya Teknolojia Dar es salaam (DIT), Chuo cha Maji (WI), Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST) na Chuo cha Ubaharia Dar es salaam (DMI)
Mashindano hayo ya Shirikisho la Vyuo vya Elimu ya Juu Tanzania (SHIMIVUTA) mwakani 2023 yanatarajiwa kufanyika jijini Tanga.
Hombolo
Postal Address: P.O.Box 1125 Dodoma, Tanzania
Telephone: +255 0652870635
Mobile: +255 0652870635
Email: info@lgti.ac.tz
Copyright ©2021 Local Government Training Institute . All rights reserved.